
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba ametoa siku 14
kwa maofisa wanaohusika na udhibiti wa dawa za kulevya kwenye mpaka wa Tunduma
mkoa wa Songwe, kuwakamata watu wanaohusika na uvushaji wa dawa hizo kutoka
nchini kwenda nchi jirani ya Zambia na nyingine zilizopo ukanda huo.
Nchemba alitoa agizo hilo jana, alipofanya ziara ya kukagua
mpaka huo, ambapo alisema ni jambo lisilofichika kuwa kwa sasa Tanzania
imechafuka kutokana na dawa za kulevya.
Alisema kutokana na Watanzania wengi kukamatwa katika nchi
mbalimbali duniani, wakijihusisha na usafirishaji wa dawa za kulevya, imefikia
hatua kwa baadhi ya nchi kufikiria kuongeza masharti zaidi kwa kila
atakayejitambulisha kuwa Mtanzania.
“Hatuwezi kuacha nchi ikachafuka kwa sababu tu ya watu
wachache.Ukienda China Watanzania zaidi ya 200 wanashikiliwa kwa dawa za
kulevya, Pakistan wapo, India, Afrika Kusini ni Watanzania. Hili linatuchafua
sana,” alisema Nchemba.
Aliutaja mpaka wa Tunduma kuwa miongoni mwa maeneo yanayoongoza
kwa kupitisha dawa hizo na kutaka nguvu kuongezwa zaidi ili kuwezesha misako.
Alisema wapo watu ambao si makondakta wa mabasi wala abiria,
lakini wamekuwa wakisafiri kila siku kwenye mabasi, hatua inayodhihirisha kuwa
ndiyo wanaojihusisha na usafirishaji wa bidhaa hizo haramu.
Alisema watu hao wamekuwa na ushirikiano na watu wengine katika
miji ya jirani, kabla ya kufika mpakani ikiwemo kijiji cha Mpemba wilayani
Momba mkoani Songwe, ambapo wakifika hapo basi husimamishwa na mzigo kushushwa,
kisha kusafirishwa kwa njia za panya hadi ng’ambo ya nchi.
“Wakati ninyi mnafanya utaratibu wa kawaida wa kupitisha gari
husika hapa mpakani, wao wanavusha kupitia njia za panya. Basi likishavuka na
mzigo unakuwa umefika Zambia wanakutana na kuupakia tena kisha wanaendelea na
safari.
“Na katika hili ni lazima mzungumze pia na wenzenu wa upande wa pili, wadhibiti pia mji unaofuata baada ya huo wa mpakani maana huko ndiko wanakopakia tena. Kama mtashindwa katika wiki mbili, nitakuja mimi mwenyewe na nitawakamata tu,” alisisitiza.
“Na katika hili ni lazima mzungumze pia na wenzenu wa upande wa pili, wadhibiti pia mji unaofuata baada ya huo wa mpakani maana huko ndiko wanakopakia tena. Kama mtashindwa katika wiki mbili, nitakuja mimi mwenyewe na nitawakamata tu,” alisisitiza.

No comments:
Post a Comment