Burundi imewapiga marufuku wachunguzi
watatu wa Umoja wa Mataifa baada yao kuchapisha ripoti wakiituhumu serikali kwa
kutekeleza ukiukaji mkubwa wa haki za kibinadamu.
Wachunguzi hao, kwenye ripoti mwezi jana, walisema maelfu ya
watu waliteswa, wakanyanyaswa kingono au wakatoweka wakati wa machafuko ya
kisiasa yaliyotokea tangu Aprili mwaka jana.
Aidha, walitahadharisha kuhusu uwezekano wa kutokea mauaji ya
halaiki kutokana na kuongezeka kwa machafuko.
Uamuzi huo wa Burundi umetokea siku chache baada ya taifa hilo
kutangaza kuwa litajiondoa kutoka Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa Kivita
(ICC).
Barua iliyotiwa saini na waziri wa mambo ya nje wa Burundi Alain
Aime Nyamitwe ilisema Pablo de Greiff anayetoka Colombia, Christof Heyns kutoka
Afrika Kusini na Maya Sahli-Fadel wa Algeria hawatakikani tena Burundi.
Ripoti waliyokuwa wamechapisha walisema kuna "ushahidi
mwingi wa ukiukaji mkubwa wa haki za kibinadamu" ambao kuna uwezekano
ukawa ni uhalifu dhidi ya binadamu, na ambao umetekelezwa na serikali ya
Burundi na watu wanaoiunga mkono.
Lakini akiongea mjini New York Jumatatu, msemaji wa UN Stephane
Dujarric aliihimiza Burundi kuendelea kushirikiana na wachunguzi wa umoja huo.
Tangazo kwamba Burundi itajiondoa kutoka mahakama ya ICC
lilitolewa wiki iliyopita miezi sita baada ya mahakama hiyo yenye makao yake
makuu mjini The Hague, Uholanzi kusema ingechunguza ghasia zinazoendelea nchini
humo.
Umoja wa Afrika (AU) mara kwa mara umeituhumu mahakama hiyo kwa
kuwabagua Waafrika.
Ghasia zilianza Burundi Aprili 2015 baada ya Rais Pierre
Nkurunzinza kutangaza angewania urais kwa muhula wa tatu.
Tangu wakati huo zaidi ya watu 500 wamefariki na wengine 270,000
kukimbilia nchi jirani.
No comments:
Post a Comment